Monday, 3 December 2018

TANZANIA BADO YAKABILIWA NA TATIZO LA LISHE KWA WATOTO CHINI YA MIAKA MITANO

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Mtoto Bibi Mwajuma Mwagwiza akielezea lengo la Mkutano  wa kitaifa wa wadau wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya Mtoto kwa mgeni Rasmi Mwakilishi wa Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto Bw. Patrick Golwike wakati wa Mkutano unaofanyika jijini Dodoma kwa  siku mbili


Mwakilishi wa Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bw. Patrick Golwike akisisitiza umuhimu wa wadau wa Maendeleo ya Mtoto kushirikiana na Serikali kuondokana na tatizo la udumavu kwa watoto kwa kupeleka elimu sahihi kwa wahusika wakati wa Mkutano wa kitaifa wa wadau wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto unaofanyika jijini Dodoma kwa  siku mbili.


Mkurugenzi wa Mtandao wa Malezi na Makuzi (TECDEN) Bw. Bruno Ghupi akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wadau wa maendeleo ya mtoto wakati wa Mkutano wa kitaifa wa wadau wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto unaofanyika jijini Dodoma kwa  siku mbili.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu Mendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bw. Patrick Golwike akisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa Maendeleo ya Jamii kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bibi Christabella  Ngowi wakati akikagua mabanda kabla ya kufungua Mkutano wa kitaifa wa wadau wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya Mtoto unaofanyika jijini Dodoma kwa  siku mbili.

Mwakilishi wa Katibu Mkuu Mendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bw. Patrick Golwike akisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa wa Maendeleo Watoto kutoka Shirika la Save the Children Bw. James Sangoro wakati akikagua mabanda ya maonesho kabla ya kufungua Mkutano wa kitaifa wa wadau wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto unaofanyika jijini Dodoma kwa siku mbili.


Baadhi ya wadau wa Maendeleo ya Mtoto nchini wakifuatilia mada na mijadala mbalimbali wakati wa Mkutano wa kitaifa wa wadau wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto unaofanyika jijini Dodoma kwa siku mbili.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano WAMJW)

NA MWANDISHI WETU DODOMA

TAKWIMU za Hali ya Watu na Afya (TDHS 2015/2016) zinaonyesha kuwa kuna tatizo kubwa kwenye lishe ya watoto  wa umri chini ya miaka 5 nchini ambapo imesababisha udumavu kwa asilimia 34 inayosababishwa na uelewa mdogo wa wazazi kuhusu kunyonyesha watoto katika muda uliopendekezwa ambapo asilimia 59 tu ya wakinamama ndiyo wanaonyonyesha watoto wao kama inavyotakiwa na asilimia 51  ya akinamama wajawazito ndiyo wanaohudhuria kliniki. Hayo yamesemwa jijini Dodoma na Mwakilishi wa Katibu Mkuu Mendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bw. Patrick Golwike wakati akiwasilisha hotuba kwa niaba ya Katibu Mkuu Dkt. John Jingu wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa kitaifa wa wadau wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto. 

Bw. Golwike amesema kuwa Serikali imechukua hatua mbalimbali katika kuboresha utoaji wa huduma za malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto kwa kuweka mazingira wezeshi ikiwemo kuandaliwa kwa Sera ya Maendeleo ya Mtoto (2008) ambayo imeelekeza utoaji wa elimu ya malezi na  makuzi kwa jamii, Sera ya Elimu na Mafunzo  (2014) inayoelekeza kuondoa vikwazo vyote vinavyomnyima mtoto haki kupata elimu na Sera ya Afya(2006) inayoelekeza utoaji wa huduma bure za afya kwa watoto walio chini ya maiaka 5 na  Sheria ya Mtoto Na. 21 ya mwaka 2009 inayoelekeza masharti ya usajili wa vituo vya kulelea watoto mchana na jinsi ya kuviendesha pamoja na Sheria ya Elimu ya mwaka 1978 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2016 ambapo inatoa adhabu ya kifungo cha miaka 30 kwa yeyote atakayesababisha mtoto kukatisha masomo.

Amesisitiza kuwa Serikali imefanikiwa kupunguza vifo vya watoto wachanga chini ya mwaka mmoja kutoka vifo 99 mwaka 2011 hadi vifo 43 mwaka 2016  kwa watoto 1,000 na katika kipindi kama hicho, vifo vya watoto chini ya miaka 5 vimepungua kutoka vifo 147 hadi vifo 67. Mafanikio haya yanatokana na maboresho yaliyofanyika katika utekelezaji wa Sera ya Afya  ya mwaka 2000.

Aidha, katika kuhakikisha kuwa watoto wote wanapata haki ya kuendelezwa kielimu, na kulindwa Serikali imehakikisha watoto wote nchini wanapata elimu bila malipo kuanzia elimu ya awali hadi kidato cha nne na imeanzisha Kamati za Ulinzi wa wanawake na watoto ambao ndio wasimamizi wakuu wa usalama wa Wanawake na Watoto na  zinaratibu vitendo vyote vya ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto kuanzia ngazi ya Taifa, Tawala za Mikoa hadi Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Ameongeza kuwa mpaka sasa Serikali imeanzisha Kamati za Ulinzi wa Wanawake na Watoto katika mikoa 26 na Halmashauri 89 kwa lengo la kudhibiti ukatili dhidi ya wanawake na Watoto bado kunahitaji msukumo zaidi ili kufikia Halmashauri zote 185 na kujenga uwezo wa Kamati hizi ili kuweza kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Nachukua fursa hii  kuwashukuru wadau  wote mliochangia kwa hali na mali kufanikisha kufanyika kwa mkutano huu na kwa namna ya pekee  napenda kuwashukuru sana Shirika la Children In Crossfire kwa kushirikiana na Mtandao wa Malezi na Makuzi (TECDEN) kwa wazo hili liliopelekea kuandaliwa kwa mkutano huu muhimu sana kwa maendeleo ya watoto wetu” alisisitiza Bw. Golwike

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mtandao wa Malezi na Makuzi (TECDEN) Bw. Bruno Ghupi ameishukuru kwa ushirikiano baina ya wadau wa Maendeleo ya mtoto na Serikali katika kuhakikisha mtoto anapata malezi na makuzi bora katika ukuaji wao ili kuwezesha kuwa na watoto wenye afya bora na utimamu wa akili.

Wadau mbalimbali wa Maendeleo ya Mtoto wanakutana Mkoani Dodoma kujadiliana kuhusu namna  bora ya kuwezesha malezi, makuzi na maendeleo ya Mtoto katika Mkutano wa kitaifa wa wadau wa malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya Mtoto unaofanyika jijini Dodoma kwa  siku mbili kuanzia tarehe 3 – 4 Desemba, 2018.

No comments:

Post a Comment