Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mhe. Abdallah Ulega akizungumza katika mkutano wa hadhara na baadhi ya
wafugaji katika Kata ya Parakuyo, Wilaya ya Kilosa Mkoani Morogoro.
……………………………………………………………………………………..
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mhe. Abdallah Ulega ameuagiza uongozi wa Wilaya ya Kilosa ya Kilosa
Mkoani Morogoro kwa kushirikiana na Meneja wa Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO)
kuwaondoa wakulima wanaolima ndani ya ranchi hiyo ya Mkata, ambao
walipewa vitalu na bila kuviendeleza, wanaokodishia vitalu wakulima na
wasiolipa kodi za Serikali.
Mhe. Ulega ameyasema hayo
Jumtatatu hii (11.12.2018) alipokuwa ranchi ya NARCO Mkata wilaya ya
Kilosa katika ziara yake ya kushughulia migogoro na malalamiko
mbalimbali ya wafugaji katika mkoa wa Morogoro.
“Nawapa mwezi mmoja kuwaondoa
wakulima wote ambao wanalima ndani ya ranchi NARCO Mkata, wale waliopewa
vitalu wakashindwa kuviendeleza pamoja na ambao hawajalipa serikali
kodi na wao waondolewe kwa mujibu wa Sheria na taratibu.” alisema Mhe.
Ulega
Katika ziara hiyo wilayani Kilosa
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega amefanya mkutano wa
hadhara na wafugaji katika Kata ya Parakuyo kijiji cha Parakuyo na
kuwaeleza wafugaji hao juu ya maagizi aliyotia kwa viongozi wa wilaya
hiyo kuhusu ranchi ya NARCO Mkata.
“Serikali ya awamu ya tano ni
sikivu na rais wetu anawapenda sana wafugaji na watu wote anatupenda, na
alishatupa maagizo wizara kuwaondoa watu waliohodhi maeneo ya ranchi na
kuwapa wafugaji wetu” alisema Mhe. Ulega
Aidha, akijibu hoja ya wafugaji
kukosa elimu ya ufugaji wa kisasa wenye tija ikiambatana na elimu ya
uzalishaji wa malisho, Mhe. Ulega aliwaagiza wataalam wa mifugo kutoka
Wakala wa Vyuo vya Elimu na Mafunzo ya Mifugo (LITA) kupeleka wanafunzi
kujifunza kwa vitendo katika kata ya Parakuyo na maeneo mengine ya
wafugaji ili waweze kusambaza elimu kwa wafugaji.
Alifafanua pia hivi karibuni
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Luhaga Mpina atazindua kampeni ya
uogeshaji mifugo ambayo itafanyika mkoani Geita wilaya ya Chato ambapo
kuogesha mifugo sasa itakuwa lazima.
Katika kampeni hii wizara inatoa
bure dawa kwa ajili ya kuogeshea mifugo na tayari zimesambazwa katika
mikoa yenye mifugo. Alifafanua dawa zilizotolewa zitaogeshea mifugo bure
kote nchini na baada ya hapo itabidi mfugaji kulipia dawa kuogesha
mifugo kila mara apelekapo mifugo yake kwenye josho.
Wafugaji hao walishukuru kwa
kutembelewa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, na kusema ujio wake
umeleta matumaini makubwa katika kumalizika kwa changamoto
zinazowakabili.
Aidha, wafugaji walimpongeza na
kumshukuru sana Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John
Pombe Magufuli kwa kuwajali na kuwatetea wanyonge pia kwa mradi wa reli
ya kisasa “Standard Gauge” ambao umewapa ajira vijana wao na pia
utasaidia katika usafirishaji wa mifugo yao kwenda katika masoko ya Dar
es Salaam.


No comments:
Post a Comment